Tuesday, 18 March

Ads Right Header

Buy template blogger

KITUO CHA AFYA CHA MAPERA KIMEPATA GARI LA KUBEBEA WAGONJWA

KITUO CHA AFYA CHA MAPERA KIMEPATA GARI LA KUBEBEA WAGONJWA
Picha na Mtandao.

KITUO cha Afya Mapera kilichopo katika Halmashauri ya wilaya Mbinga mkoani Ruvuma, kimepata gari la wagonjwa(Ambulance) iliyonunuliwa na Halmashauri hiyo ili kurahisisha usafiri kwa wagonjwa watakohitaji na kupewa rufaa kwenda Hospitali ya wilaya Mbinga na Rufaa  ya mkoa Songea.

Akikabidhi gari hilo kwa Mganga Mkuu wa kituo cha Afya Mapera,Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Juma Mnwele alisema, gari hilo limetokana na ahadi iliyotolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa wananchi wa kata ya Mapera la kuwapatia gari la wagonjwa kwa ajili ya kituo hicho.

Alisema, Waziri Mkuu baada ya kupata ombi hilo aliiagiza Halmashauri ya wilaya kutumia mapato yake ya ndani kununua gari la wagonjwa kwa ajili ya kituo  cha Afya Mapera ili lisaidie wananchi hasa wagonjwa watakaopewa rufaa kutoka katika kituo hicho kwenda Hospitali  ya wilaya Mbinga mjini,au Hospitali ya Rufaa ya mkoa Songea kwa ajili ya matibabu zaidi.

Mnwele alisema,gari hilo limenunuliwa kwa shilingi ml 138 kutokana na fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri ambapo  linakwenda kumaliza kero ya wagonjwa wanaopewa rufaa kukodi magari ya watu binafsi  kwa gharama kubwa ikilinganisha na hali  halisi ya maisha ya wananchi hao.

Alisema, katika mkoa wa Ruvuma kuna vituo vya Afya 16 lakini ni  Mapera ndiyo iliyopewa upendeleo kwa kupata fedha za kujenga majengo mapya  katika kituo cha Afya na kupata gari jipya la wagonjwa.

Hata hivyo alisema,  kwa kuwa halmashauri ya wilaya Mbinga ni kubwa  kuna wakati litahitajika kwenda kutoa huduma kwa wagonjwa wa vijiji vingine  katika halmashauri hiyo, na kuwaeleza wananchi kwamba gari hilo litatumika kwa ajili ya wagonjwa na sio  shughuli nyingine za kijamii.

Akizungumzia ujenzi wa majengo hayo alisema,  Serikali kuu imetoa shilingi ml 500  na Halmashauri ya wilaya imeongeza milioni 80  zilizowezesha kukamilisha kazi ujenzi huo ambapo ameishukuru Serikali kwa  kutoa fedha hizo  ambazo zimekwenda kuimarisha na kuboresha huduma za matibabu kwa wananchi.

Alisema, kujengwa kwa  majengo mapya  kutawezesha wauguzi na madaktari kufurahia mazingira bora na hivyo kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa.

Alisema, mbali na kununua gari na kuongeza  majengo mapya,Serikali  imepeka Madaktari wawili ambao watasaidiana na waliopo kutoa huduma za matibabu na kuwataka wananchi wa Mapera kuwapa ushirikiano ili waweze kutekeleza wajibu wao.

Baadhi ya wananchi  Betram Komba,Anitha Nikata na Mganga Mkuu wa kituo hicho Dkt Charles Sanga wameipongeza Halmashauri ya wilaya Mbinga kwa kuona umuhimu wa kununua gari la wagonjwa  na kutekeleza haraka agizo la Waziri Mkuu  Kassim Majaliwa.

Betram Komba Alisema, awali kulikuwa na changamoto ya  gari la wagonja pale mgonjwa anapohitaji rufaa kwenda Hospitali kubwa kwa ajili ya huduma kama ya upasuaji kwani walilazimika kukodi magari ya watu binafsi kwa gharama kubwa jambo lililopelekea baadhi ya wananchi kushindwa kumudu gharama  ya kukodi magari.

Alisema,hali hiyo ilisababisha baadhi ya wananchi hasa akina mama wajawazito kujifungulia njiani na wengine kupoteza maisha kwa kushindwa kufika kwa wakati katika Hospitali kubwa.

Leave Comments

Post a Comment

Ads Post 4