Wazazi Ondoeni Muhali kwenye kesi za udhalilishaji

CHAMA cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA, ZNZ) kinawaomba wazazi na walezi kuacha tabia ya kuficha matukio ya udhalilishaji ambayo wamefanyiwa watoto ndani ya jamii, kwani kuendelea na tabia hiyo kunapelekea kusabisha wimbi kubwa la wahalifu wa matukio ya udhalilishaji hapa Zanzibar.
Kuendelea kuwepo kwa wazazi na walezi wenye tabia ya kuficha matukio hayo baada ya mtoto kufanyiwa vitendo vya kubakwa au kulawitiwa ni kuathiri kasi kubwa ya maendeleo ya wanawake na mipango ya nchi katika kupambana na vitendo vya udhalilishaji nchini. Pia ni njia moja wapo ya kuwapa mwanya watu waovu kuendelea kuwafanyia watoto vitendo viovu.
Hivi karibuni mtandao wa kupambana na ukatili wa kinjisia kwa wanawake na watoto wa Wilaya ya Mkoani Pemba, umesema umepokea taarifa kwamba mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Salmini Musa Juma (29) mkaazi wa Jombwe shehia ya Muambe Wilaya ya mkoani, Kusini Pemba, anadaiwa kuwabaka watoto watatu, ambapo kati yao wawili wakiwa na umri wa miaka tano (5) na mmoja mwenye umri wa miaka sita (6). Tukio hilo limetokea Agosti 25 katika Shehia hiyo.
Mratibu wa TAMWAZNZ kwa upande wa Pemba, Fat-hiya Mussa Said amesema amepokea taarifa kutoka kwa mtandao huo umebainisha kwamba kati ya matukio hayo ya kuwadhalilisha watoto watatu ni matukio mawili tu ndio yameripotiwa katika kituo cha polisi cha Kengeja, Mkoa wa Kusini Pemba, huku tukio moja likiwa halijaripotiwa kutokana na muhali ndani ya familia kwa kuwa mtuhumiwa ana uhusiano na mtoto aliyembaka.
Mratibu huyo amesema mtandao unaendelea kuwashawishi wanafamilia hiyo waondoe muhali na kuchukua hatua ya kuripoti tukio hilo katika kituo cha polisi ambapo pia mtandao unaendelea kuziunga mkono familia mbili zilizoripoti matukio hayo ili kutovunjika moyo na kuacha kufuatilia kesi katika vyombo vya sheria.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka jeshi la Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba, mtuhumiwa wa matukio hayo anakabiliwa na makosa mawili kosa la shambulio la aibu na kumwingilia kinyume na maumbile mtoto wa kike.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kusini Pemba, Ahmed Khamis Makarani amesema tayari kesi hiyo imeshakamilisha upelelezi wake na jalada limepelekwa kwa Murugenzi wa mashataka kwajili ya kuendelea na hatua inayofuata.
Kutokana na hali hiyo, TAMWA ZNZ, kinaendelea kuwashauri jamii kuacha tabia za kuwalinda wahalifu kwani kufanya hivyo kutaongeza idadi ya uhalifu huo nchini pamoja na kuwaweka watoto na wanawake katika hofu kubwa na kutokuwa na imani kwa jinsia ya kiume.
Aidha TAMWA ZNZ inaviomba vyombo vya sheria vilivyosalia kulipa shitaka hilo uzito unaostahiki ili kukomesha vitendo hivyo viovu nchini.
Previous article
Leave Comments
Post a Comment