SEPTEMBER 1 SEHEMU YA PILI

Chagua moja, urudi nimwage ubongo wake, au uongozane na makomadnoo hapo waliyokuja kukupokea", Kauli ilimfanya mwenyewe afuatane na makomandoo wa hapo chuoni.
**
Majira hayo jijini Dar es salaam, jasusi na mwandishi wa habari wa kujitegemea Norbert Kaila alikuwa yupo nyumbani kwa Belinda. Majira ya nchini Cuba yakionesha ni saa moja asubuhi muda aliyowasili Benjamini, huku ilikuwa ni saa tano usiku. Muda huo kijana huyu machachari alifika nyumbani hapo, akiwa na lengo moja tu la kujadliiana juu ya ziara yake ya kiuandishi wa habari.
Jeshi la wananchi wa Tanzani lilichukua dhima ya kumaliza ujenzi wa reli ya SGR hadi jijini Mwanza baada ya hatua za awali kumalizika, kijana huyu alihitaji kwenda kujionea jinsi mambo yanavyoendelea. Namna maafisa wa jeshi wanvyochakarika kutimiza jukumu lao la kizalendo, ndiyo maana alikutana na mnadhimu mkuu wa majeshi nchini majira hayo yaani Luteni jenerali Belinda.
"Nor hii ni safari au kuna jingine la ziada hebu niambie", Belinda aliuliza.
"Ni safari ya kuionesha dunia kupitia kazi yangu, jinsi ambavyo jeshi la wananchi wa Tanzani lilivyojitolea kuweza kukamilisha kazi hii", Norbert alijibu.
"Nor usinifiche kama kuna jingine la ziada naomba unieleze tu, ukumbuke kuna maafisa wanne wa kikosi cha kutegua mabomu wamepotea juzi tu na hawakuonekani. Usije ukawa unaenda kuchunguza huko na ukaanika gazetini, Afande Marwa hawezi kunielewa ikiwa itatokea habari hii ikavuja kwenye vyombo vya habari, MI wapo kazini kushughulikia hili"
"Belinda! Belinda! Toka lini nikakuficha usiweze kuelewa chochote kile kuhusu mipango yangu. Mmoja kati ya watu wanaoujua uhalisia wangu ni wewe nitaanza vipi kukuficha, vya kukuficha vipo ila si hiki"
"Mh! Ok haya niambie cha kunificha ni kipi kikubwa zaidi ya hiki"
"Kuchukua goma Norene asijue ndiyo cha kukuficha, au nikuibie Vero"
"(Akicheka) Hivi wewe utaacha lini kupenda sketi, umri unaenda huo mtoto wako anafikia miaka ya karibuni tu. Ila baba mtu bado upo na sketi"
"Mamba akiacha kuwinda mtoni, nami nitaacha. Hebu tuachane na hayo, nahitaji ruhusa haswa wale hawanitambui nisije nikachezea kichurachura juu ya reli tu nikibebeshwa mataruma"
"Ok kama lengo lako ni kulitangza jeshi kimataifa zaidi, hakuna jinsi zaidi ya kukuruhusu tu.
Wasiwasi wangu ulikuwa ni huo tu, maana wewe ulivyo mfukunyuku kama Panya, ruksa ipo kesho fika kambini utaenda na helikopta na kukagua eneo lote la reli na kulitangaza jeshi la nchi yako"
"Hapo sawa naipenda Tanzania, daima nitaitangaza tena safari hii mlivyoamua kuchukua jukumu hili na kuwafanya wakandarasi walafi wakose kitu. Kuna haja ya kuwapongeza, ingawa mwanzo wanasiasa wa upinzani waliponda kitu hicho"
"Vyema sana, lazima jukumu kama hilo likabidhiwe kwetu angalau mainjinia wapo kambini tu hawana kazi ya nini waletwe wa nje. Hao wanasiasa waache waendelee kupiga porojo zao, tukija kumshika mmoja atakuwa mfano. Suala la maendeleo wao
wanataka kulitia najisi, nadhani mkwara wa msemaji mkuu unawatosha kabisa"
"Sawasawa kwa pamoja tutaijenga na kuisimamisha nchi daima"
Norbert hakudumu nyumbani kwa Belinda, aliondoka usiku huohuo kurejea kwake kwenda kujipanga kwa ziara ya maeneo ambayo wanajeshi wanafnya kazi yao ya kujenga reli ya kisasa baada ya hatua za awali kukamilika.
**
Mwezi mmoja baadaye jarida lenye kuonesha kila eneo ambalo jeshi limefanya akzi, lilisambaa sehemu mbalimbali nchini na kupelekea watanzania wengi wajisifu kuwa na jeshi lenye kujituma zaidi kwenye nyanja mbalimbali za kimaendeleo.
Wanasiasa wale wenye kutafuta la kuongea hata mahali ambapo kwenye wema, walikaa kando juu ya hili kutokana na kushikwa na kikosi kisichotaka lolote kuhusu siasa liingie kazini kwao. Jambo hili lilipelekea Kaila apewe pongeze kubwa kutoka ndani ya jeshi, kiasi cha kuweza kumtunuku pongezi maalum kwa ajili ya kazi yake hiyo. Kwani vituo mbalimbali vya habari kutoka sehemu mbalimbali duniani, vilizungumzia kuhusu suala lile.
Lilikuwa ni mwiba mno kwa upinzani wenye kutafuta nafasi ya kuisema serikali, ili waweze kujiwekea nafasi nzuri ukifikia uchaguzi. Jambo hilo na makubwa mengi yaliyofanyika chini ya Rais Zuber Ameir, yalipelekea hata kiongozi yule aambiwe anaweza kugombea zaidi na zaidi kama watabadili katiba ya nchi hiyo. Ila ndiyo hivyo aliheshimu sheria, akatangaza mapema zaidi hatokuwa tayari kugombea hata kama sheria hiyo ikipita.
**
Miaka miwili na nusu baadaye ndipo Benjamini aliporejea nchini Tanzania, muda hu akiwa ni mwenye mafunzo makubwa ya kijeshi na mwenye uwezo mkubwa wa kupambana kinamna yeyote ile. Aliwasili uwanja wa ndege jijini Dar es salaam, ambapo alipokewa na mfadhili wake na akapelekwa moja kwa moja hadi kwenye nyumba ya kifahari ambayo aliahidiwa kupewa ikiwa angerejea nchini akiwa kahitimu mafunzo hayo.
Huko alikutana na mtu mwingine ambaye hakuwahi kumtia machoni kabla, alikaribishwa kwenye kochi la kisasa na mizigo yake aliyokuja nayo iliingizwa ndani.
"Benjamini Simon Mluva karibu tena kwa mara nyingine nchini, kuanzia sasa tambua jina lako la kikazi ni Besi yaani ikimaanisha BEnjamini SImon. Hilo ndiyo mmoja wetu atakuita ikiwa kuna kazi, atakayekuita jingine hesabu si miongoni mwetu", Mfadhili wake alisema.
"Kwanza Mr Watson nahitaji kujua tu lengo la kunipa mafunzo yale na kufadhili kila kitu ni nini haswa?", nBenjamin aliuliza.
"Ndiyo mwanzo wa kazi yenyewe hiyo kijana, ukae ukitambua pea si rahisi sana kuishika bali inahitajika uitolee jasho. Kuanzia hivi sasa jua wewe ni mwajiriwa wa Kibolongo investment company, huyu aliyepo mbele yako ndiye mkurugenzi mkuu wa kampuni yenyewe anaitwa Kibolongo. Hiyo ni sehemu ya kazi yako itakayotambulika uraiani. Nadhani wewe mwenyewe
unajua kazi yako halisi ni ipi?"
"Iam The Bomb engineer"
"Safi sana, sasa tambua hiyo kazi ina muda wake maalum. Nadhani kile ulichojifunza ni muda mwafaka kwa kukiafanyia kazi, je una huruma na kiumbe yyote kwa sasa?"
"Siwezi kuwa na huruma na mtu hivi sasa, mliponipelekea mmenipandikiza roho ya paka"
"Hivi ndivyo Alpha alitaka uwe, unatakiwa utambue mkuu wetu sisi sote hapa anaitwa Alpha. Huyo ndiye aliyeweza kulipia masomo yako yote, na pia ndiyo anatulipa sisi hadi ukaona tuna maisha mazuri. Nawe amekukabidhi nyumba hii kama mwanzo wa ahadi yake aliyoitoa kwako, ambayo nilikuja kama mimi kujifanya nimekuahidi. Besi tambua mkuu anakupenda sana haswa baada ya kupata sifa zako mafunzoni, usijaribu kumwangusha"
"Nitaanza vipi wakati ndiyo amenipa kile nilichokuwa nikihitaji, sasa hivi ninaonekana mtu mbele za watu"
**
Majira hayo Norbert yupo katikati ya jiji akiongozana na binti mrembo, kijana ahuyu mwenye kupenda kufuata mabinti kila wamvutiapo. Alijikuta akiunga mkia kwa banati mrembo huku akiendelea kutumia sumu ya ulimi, na kumfanya binti yule aliyekuwa na kasi aende taratibu sambamba naye kusikiliza maneno ampayo. Hatimaye aliweza kumfanya binti hata ashindwe kuweka pingamizi kila autazamapo uso wake, uliyojaa silaha yake kubwa ambayo ni bashasha. Ambayo humfanya mrembo akioneshewa basi awe hana uwezo wa kumkazia, ndiyo maana aliwanasa wengi mno.
Kaila pamoja na kuwa umri umeanza kumkimbia akiwa bado yu ndani ya ujana wake, sura yake na haiba yake haikuwa imemtoka hata. Ndiyo kwanza alivutia mno, hata mrembo huyo akajikuta akisimama na kuongea naye jirani na maegesho ya magari.
Akiendelea kumchombeza hakutilia maanani gari lenye vioo vya giza lililopo mahala hapo, hadi mlango ulipokuja kufunguliwa na kumwona aliyepo ndani ya chombo kile. Alijikuta akimwaga binti huyo na kuahidi angewasiliana naye, hata teksi alimchukulia ilimradi aondoke mahala hapo.
Binti alipotoweka ndipo aliporejesha macho kwenye mlango wa gari, akiwa namna hiyo moyoni alilaani mno kwa kufunguliwa mlango ule.
"Unashangaa nini wewe Kapera, inga garini haraka sana", Mtu aliyepo ndani ya gari alimwamuru, naye hakuwa na pingamizi.
"Naona umekuwa kama chatu, tabia ya kumeza mawindo huiachi kamwe ingawa umefikia umri wa kuitwa baba", Aliambiwa alipoingia ndani ya gari na sauti itokayo nyuma yake ilisikika, huko kulikuwa na mtu mwingine tofauti na yule wa awali.
Alipogeuza uso kutazama huko, ndipo alipokutana uso kwa uso na CE. Hapo akajua ameonekana hila zake zote alizozifanya kwa binti yule, tena kibaya zaidi bosi wake ni mwenye kumjua kiundani juu ya tabia yake ya ukware. Hata angeandaa la kujitetea lisingesaidia maana aliona kila kitu. Waliyosema aonaye mengi hadanganywi, hawakukosea. Mzee huyu kwenye umri wake na kazi yake ameshuhudia kila aina ya kioja, pia amezikairi kila tabia za vijana wake. Norbert angeanzia wapi kumwongopea, ilihali uongo kwa mkuu wake wa kazi ni mwiko.
"Umepigiwa simu ya ofisini haupatikani, umepigiwa simu ya mkononi kupokea ukaona tabu kumbe upo na bibie yule. Tumekunasa location yako kupitia simu yako ndiyo maana tukafika hapa. Tena vyema umekuja mwenyewe", CE alisema akiwa kiti cha nyuma kabisa kwenye gari hiyo iliyofanana kila kitu na noah ila haikuwa mali ya kiwanda cha toyota. Mkuu huyu alinyoosha mkono wake wenye bahasha akampaia Norbert, ambaye naye aliifungua kwa utulivu mkubwa akatoa picha zenye kuonesha maafisa mbalimbali wa kijeshi.
"Hawa ni kutoka bomb squad ndani ya JWTZ, kazi yao kubwa nadhani unaijua. Kikosi kile ndani ya jeshi hakuna mwenye uwezo kuwazidi hawa katika uteguaji mabomu, ni mainjinia wa kutegemewa kwenye kazi ile. Waliyobaki huko kambini ni wasaidizi wao tu, ila wakuu wenyewe ni hawa", CE alisema kisha akanyoosha mkono wake ambao una faili, aliufikisha kwenye bega la Norbert. Ambaye alipokea jalada hilo lenye kutunza kumbukumbu mbalimbali. Mkuu wa kazi aliendelea, "N001 ukae utambue hivi sasa mainjinia wote wa bomb squad hawajulikani walipo, hilo faili lina kila kitu chao kiundani zaidi. Sijui walipo na wewe hujui walipo, kiufupi tuliyopo humu ndani hakuna anayejua ni walipo. Sasa basi unahitajika kujua walipo ndani ya mwezi huu wa Agosti, septemba tatu hakikisha wanapatikana wote. Kazi ya jeshi ni kulinda mipaka ya nchi hii kinamna yeyote, kwenye hili ilihitajika ishughulike MI ila tumepokea kijiti kuwasaidia. Je una swali?"
"Utambulisho wangu kwenye suala hili upo namna gani?", Norbert aliuliza.
"Kama ulivyoweza kufanikisha kupatikana kwa Gera, atakayeiona sura yako halisi kama N001 basi hakikisha hawezi kuishi salama lazima awe mikononi mwetu kukulinda uhalisia wako kazini. Kama ulivyovaa sura bandia ulipokutana kwenye kikao na Timothy, mwenye kukujua asiyekuwa mwanausalama basi aingie kwetu tu"
"Sina jingine la ziada, nitahitaji muda wa kuilaza akili ya Norbert ili N001 aamke na kuingia kazini tu", Alipoongea hivyo, Afisa wa EASA aliyekaa mbele alimpatia mkoba wa namba mkubwa tofauti na ile iliyozoelea kuwekewa fedha.
"Humo ndani kuna vitendea kazi, kuanzia mavazi, kiatu na hadi kofia. Miwani pia ipo na hadi silaha utakazoitajika kuzitumia. Kazi ikamilike kuendana na muda uliyopewa........N001 hujawahi kuniangusha na sitaraji kutokea hilo nikutakie kazi njema", CE aliongea. "Angalia upande wa pili wa parking hii, nadhani unaiona ile BMW nyeusi. Ni gari yenye kutumia gesi na si mafuta, ina mfumo wa gia wa manual na pia una auntomatic. System yake ni umeme yote, hiyo ndiyo gari utakayoitumia kuanzia mwanzo hadi mwisho wa misheni hii. Ina credential, haiwezi kuwaka bila kupata alama ya kiganja cha authorized. Funguo ni hizi, kila la heri", Afisa aliyempatia mkoba kwa mara ya kwanza alimwambia huku akimkabidhi funguo za gari.
"Asante sana kwa jeti ya ardhini", Norbert alisema huku akipokea ufunguo, alishuka akiwa na mizigo yake yote na lango la gari lile lilifungwa. Kwa mwendo wa taratibu alianza kutembea kuelekea upande wa pili maegesho yale hadi akafika kwenye gari ya kisasa aliyoelekezwa.
"Kazi za kufa wananipa vitu kama hivi, muda wa starehe natumia mikweche yangu. Damn!", Alisema huku akifungua mlango wa dereva akaweka mafaili na picha kiti cha pembeni, alifungua eneo la mizigo la gari hiyo kisha akaweka mkoba wake.
Alipofunga eneo la mizigo kuja kurejea mbele, alikutana na binti yule aliyetoka kumchomeza muda mfupi uliyopita. Alishangazwa haswa na ujio wake mahala hapo, ilihali waliagana naye na kusema wangewasiliana. Kaila alibaki ameduwaa tu akimtazama, shaka yake ikiwa ni juu ya faili ambalo lipo kwenye kochi la abiria ndani ya gari hiyo.
Alihisi lingeweza kuonekana na binti huyo, pia mkuu wake ambaye aliegesha gari mita chache kutoka hapo naye angeweza kumwona. Alipoangaza macho kule alipokuwa hapo awali, aliona ni kweupe na hakujua gari ile aliyokuja nayo CE iliondoka muda gani.
Alishusha pumzi na akapiga hatua kumsogelea binti huyo, akiweka uso wa kujiamini pamoja na tabasamu kwa mbali ili asimpe nafasi ya kuendelea kuwaza kingine zaidi. Alijua wazi angeshughulika kumtazama usoni, jambo hilo lingekuwa ni silaha tosha nyingine ya kuweza kumtuliza.
"Mr Smile, sikuelewi na mizigo yako hiyo unaenda nayo wapi? Umekuja mikono mitupu ila hivi sasa unatoka na mizigo na kuingia kwenye luxury car kama hii, Nor kumbe umeniondoa ilimradi uingie mule tu kwenye tinted", Binti aliongea.
"Halima mbona upo hapa? Si nilikuchukulia gari ukaondoka?", Norbert aliuliza.
"Ulitegemea ningefanya nini kama si kurudi hapa, si uliniahidi utanichukua na kwend lunch. Kwanini ubadilike namna ile, kisa hiyo tinted. Nor una mwanamke mwingine mule ndiyo maana ukaniondoa hapa", Binti alipokuwa akilalamika hayo, Kaila alichukua wasaa wa kuchukua mafaili yote alipoufikia mlango wa dereva na kuyaingiza kwenye saraka iliyopo ndani ya gari kisha akafunga.
"Dah! Wanawake wengine hawa kama si pepo hili ni nini, mtu ndiyo nimemtongoza tu tayari keshajawa na wivu na kuona ananimiliki. Jibu lenyewe hakulitoa", Norbert alijisemea moyoni huku akiketi kwenye kochi na akamtazama Halima aliyesimama wima akiona kama kapuuzia maneno yake. Alimuuliza, "Halima wasiwasi wako ni upi kwani, hivi kwa akili yako mimi kuonana na mwanamke ningekuja hapa kweupe na kuingia ndani ya gari. Jaribu kufikiria kabla hujanituhumu kisura, mimi ni mwandishi wa habari hujui ninakutana na wangapi kinamna gani kwa ajili ya kazi zangu"
"Ndiyo uniondoe mimi?"
"Sasa ningefanyaje, kama ingekuwa ni hatari ya kuhatarisha maisha yako, nitakuwa kiumbe wa aina gani mimi niliyemuhusudu mrembo kwa dakika chache
zilizopita nije kumtia hatiani. Habibu wa moyo wangu ni wa kumwepusha, shari ijayo kwangu ishindwe kumkumba"
"Ok, sasa tunaenda wapi sasa hivi Nor, yaani hapa ile ahadi uliyoniahidi wakati tunatembea lazima itimie"
"Ok twende hotelini sasa hivi ukapate hadi chakula cha mchana ndiyo tweondoke huku"
Ilimbidi Kaila akubali kuondoka na binti huyo, tena akampakia ndani ya gari ambayo amepewa kwa ajili ya kufanyia kazi. Angeanza kumkatalia na msichana ndiyo kageuka ruba baada ya kuona gari la kifahari alilonalo kijana huyo.Pia jina kubwa alilojitengenezea Norbert kwenye uandishi wa habari ndiyo lilimfanya aone ni bahati ya mtende hiyo, angeanza vipi kumwacha aondoke tu na alimpa ahadi tamu kipindi anaongozana naye.
ITAENDELEA
NAFASI MPYA ZA KAZI KWA WENYE ELIMU KUANZIA DARASA LA SABA ,KIDATO CHA NNE,CERTIFICATE,DIPLOMA,DEGREE NA KUENDELEA ZIPATE KUPITIA AJIRA FORUM APP 👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇👇
Previous article
Next article
Leave Comments
Post a Comment